Utafiti JKCI wachambua uhusiano kati ya dawa za moyo za SGLT2i na Afya ya njia ya mkojo
-
Author: JKCI Admin
-
Published At: Tuesday, Apr 14, 2026
Utafiti mpya uliofanyika katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) jijini Dar es Salaam umebaini kuwepo kwa ongezeko la maambukizi ya njia ya mkojo (UTI) miongoni mwa wagonjwa wa moyo wanaotumia dawa aina ya Sodium-Glucose Co-Transporter 2 Inhibitors (SGLT2i) zikiwemo dapagliflozin na empagliflozin.
Dawa hizo ambazo zimekuwa msaada mkubwa katika matibabu ya magonjwa ya moyo na figo sasa zinaibua mjadala mpya kufuatia kuhusishwa na hatari ya kuongezeka kwa maambukizi ya UTI kwa baadhi ya wagonjwa.
Utafiti huo uliofanywa na Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa JKCI Dar Group Samueli Rweyemamu kwa kushirikiana na wataalamu wenzake na kuchapishwa katika Jarida la PLOS ONE la nchini Marekani uliendeshwa kwa kipindi cha miezi mitatu kuanzia Machi hadi Juni 2024. Ulihusisha jumla ya wagonjwa 141 wenye umri wa miaka 18 na kuendelea waliokuwa wakitumia dawa za SGLT2i.
Akizungumza na mwandishi wa habari hii jijini Dar es Salaam Dkt. Rweyemamu alisema lengo kuu la utafiti huo lilikuwa ni kubaini kiwango cha maambukizi ya UTI, sababu zinazochangia maambukizi hayo pamoja na uhimilivu wa vimelea dhidi ya dawa za antibiotiki kwa wagonjwa wa moyo.
Alifafanua kuwa matokeo ya utafiti yanaonesha kuwa kati ya sampuli 138 za mkojo zilizopimwa wagonjwa 22 sawa na asilimia 15.9 walikutwa na maambukizi ya njia ya mkojo.
“Idadi hii ni kubwa ikilinganishwa na tafiti za awali ambazo zilionesha viwango vya chini zaidi vya maambukizi kwa watumiaji wa dawa hizi”, alisema Dkt. Rweyemamu.
Kwa mujibu wa utafiti huo, vimelea vilivyobainika kusababisha maambukizi hayo kwa kiwango kikubwa ni pamoja na Escherichia coli (asilimia 50), Klebsiella pneumoniae (asilimia 13.6), Pseudomonas aeruginosa (asilimia 9.1) na Candida spp. (asilimia 9.1).
Dkt. Rweyemamu alieleza kuwa vimelea hivyo huathiri zaidi watu wenye kinga za mwili dhaifu wakiwemo wagonjwa wa moyo na kisukari hali inayoongeza uwezekano wa kupata maambukizi ya mara kwa mara.
Utafiti huo ulibaini kuwa baadhi ya makundi yako kwenye hatari kubwa zaidi ya kupata UTI yakiwemo ya watu wenye umri wa zaidi ya miaka 60, wanawake, pamoja na wagonjwa wanaotumia dawa za SGLT2i kwa muda mrefu zaidi ya miezi minne.
Alibainisha kuwa sababu kuu inayochangia hali hiyo ni glycosuria—uwepo wa sukari kwenye mkojo unaosababishwa na matumizi ya dawa hizo. Sukari hiyo hutoa mazingira rafiki kwa bakteria kuzaliana kwa haraka ndani ya mfumo wa mkojo na hivyo kusababisha maambukizi yanayoweza kuwa ya kawaida kama cystitis au makali zaidi kama pyelonephritis na urosepsis.
Kuhusu matibabu utafiti umeonesha kuwepo kwa usugu mkubwa wa vimelea dhidi ya baadhi ya antibiotiki ikiwemo ampicillin (asilimia 100), tetracycline (asilimia 69.2) na ceftazidime (asilimia 53.8).
Hata hivyo, dawa kama nitrofurantoin zimeonesha ufanisi mkubwa, ambapo asilimia 84.6 ya vimelea vilionekana kuwa nyeti huku meropenem ikionesha ufanisi wa asilimia 100.
Kutokana na hali hiyo, Dkt. Rweyemamu ambaye pia ni Mkuu wa Huduma za Tiba, JKCI Dar Group alisisitiza umuhimu wa wagonjwa wa moyo kufanyiwa uchunguzi wa mkojo kabla ya kuanza tiba ili kuhakikisha wanapatiwa dawa sahihi kulingana na aina ya maambukizi.
“Matokeo haya yanatoa tahadhari kwa wataalamu wa afya dhidi ya matumizi ya dawa bila kuzingatia usikivu wa vimelea, jambo ambalo linaweza kuchochea tatizo la usugu wa dawa changamoto ambayo tayari inaongezeka katika ukanda wa Afrika Mashariki ikiwemo Tanzania” alionya.
Utafiti huo pia umeweka mkazo katika umuhimu wa uchunguzi wa mara kwa mara kwa wagonjwa wa moyo wanaotumia dawa za SGLT2i, hususan kwa wazee na wanawake, ili kubaini maambukizi mapema na kuyatibu kabla hayajawa makubwa.
Aidha, umehimiza kuimarishwa kwa sera za kitaifa za kudhibiti usugu wa viuavijasumu pamoja na kuboresha huduma za maabara nchini kwaajili ya uchunguzi sahihi wa maambukizi ya UTI.