• P.O Box 65141
  • +255-788-308999

Raia wa Malawi avutiwa na huduma bora za moyo JKCI, atoa shukrani za dhati

  • Author: JKCI Admin
  • Published At: Tuesday, Sep 09, 2025
image description

Mkazi wa Blantyre nchini Malawi Enita Dinnot-Phiri ameishukuru Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kutoa huduma bora za kiwango cha kimataifa za matibabu ya kibingwa ya moyo kwa watanzania na wasio watanzania .

Shukrani hizo amezitoa hivi karibuni wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kufurahishwa kwake na huduma za matibabu ya moyo alizozipata katika taasisi hiyo.

Enita alisema mara baada ya kugundulika kuwa na tatizo la moyo alipewa nafasi ya kuchagua nchi ya kwenda kutibiwa ikiwemo India lakini yeye alichagua kwenda Tanzania katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) mahali ambapo amepata matibabu ya kiwango cha juu.

“Nilifika hapa Jumamosi iliyopita  na nilijua kwamba huenda nikapatiwa matibabu siku za kazi yaani kuanzia Jumatatu, lakini baada tu ya kupokelewa kutoka Airport nilianza kupatiwa matibabu ambayo kwakweli sikutarajia kuyapata nimefurahi sana”.

“Namshukuru Mungu nimepata matibabu na nimeruhusiwa, ninawapongeza wafanyakazi  wote wa taasisi hii  kwa moyo wao wa ukarimu na upendo kwani kazi yao wanayoifanya ya kuokoa maisha ya watu ni kubwa na wanastahili kupewa pongezi”, alishukuru Enita.

Kwa upande wake Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dickson Minja alisema walimpokea Enita kutoka nchini Malawi ambaye alikuwa na changamoto ya moyo iliyohitaji kupata huduma ya matibabu ya haraka.

Dkt. Minja alisema kutokana na uhitaji wa haraka wa huduma ya matibabu kwa mgonjwa huyo siku ya Jumapili kwa kutumia mtambo wa Cathlab walimfanyia upasuaji wa moyo wa bila kupasua kifua ambao ulikwenda vizuri bila ya changamoto yoyote.

“Ninawaomba wananchi wenye matatizo ya moyo wafike katika taasisi yetu ili wapate matibabu kwa wakati kwani muda wote hata siku za sikukuu tunatoa huduma za matibabu ya viwango vya ubora wa kimataifa hii ni kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa na serikali yetu kupitia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.